Meneja wa Statoil Tanzania, Oystein Michelsen
Kampuni ya Statoil na mshirika wake, Exxon Mobil, imetangaza matokeo
mazuri ya majaribio ya gesi kwenye kitalu namba mbili katika kina kirefu
cha bahari kisima cha Zafarani-2.
Kwa mujibu wa Meneja wa Statoil Tanzania, Oystein Michelsen, majaribio
hayo kwenye kisima cha Zafarani-2, kimeonyesha kuwa na uwezo wa
kutiririsha futi za ujazo milioni 66 kwa siku.
Alisema takwimu zilizopatikana kwenye majaribio hayo, ni muhimu kwa
ajili ya kupunguza shaka inayoweza kuwapo siku za usoni kuhusu gesi
iliyoko ya kina kirefu cha bahari na gesi ya kusindikwa hapa nchini.
Alifafanua kuwa majaribio ya uchimbaji yalifanywa katika kisima cha
Zafarani-2 urefu wa mita 2,400 ndani ya kina kirefu cha bahari na ikiwa
ni umbali wa kilomita 80 kwenda nchi kavu.
Alieleza kuwa baada ya majaribio ya kisima cha Zafarani-2 , kutafuatia
uchunguzi wa kiwango cha gesi kwenye kisima cha Zafarani-3, ambacho
ndicho cha mwisho kwenye utafiti katika hifadhi ya gesi kwenye kitalu
namba mbili.
Alisema kutangazwa kwa matokeo ya majaribio ya kisima cha Zafarani-2
kunafuatia ugunduzi kwenye kisima cha Mronge-1 kulikofanyika Desemba
2013, ambako kunafanya ugunduzi huo kuwa kisima cha tano kwa utafiti
unaofanyika kwenye kitalu namba 2.
Alisema ugunduzi huo umefanya jumla ya kiasi cha gesi iliyogundulika kufikia futi za ujazo wa kati ya trilioni 17-20 (Tcf).
Alisema kabla ya ugunduzi uliotokea kwenye kisima cha Mronge-1 kulikuwa
na ugunduzi mkubwa gesi wakati wa uchimbaji wa awamu ya kwanza kwenye
kisima cha Tangawizi-1, Zafarani-1 na Lavani-1, na ugunduzi mwingine
kwenye kisima cha Lavani-2.
Kampuni ya Statoil ina leseni ya kufanya utafiti katika kitalu namba
mbili kwa niaba ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC),
ikiwa na asilimia 65 wakati mbia wake kampuni ya ExxonMobil Exploration
and Production Tanzania Ltd ikichukua asilimia 35.
Kampuni ya Statoil imekuwa Tanzania tangu mwaka 2007, ilipopewa leseni
na serikali kwa ajili ya kufanya utafiti kwenye kitalu namba 2.
VIA: NIPASHE